Friday, September 20, 2024

QUEEN SOPHIE” ASHIRIKI MAADHIMISHO YA SIKU YA NTDs NA MAFANIKIO YA “BILIONI 12 KWA AJILI YA DAWA ZA NTDs” ZANZIBAR


WAZIRI wa Afya Nassor Ahmed Mazrui, akiwa na Mwanamfalme wa Uiengereza Sophie Helen wakipokelewa na wanafunzi wa Skuli ya Kinuni A waliposhiriki maadhimisho ya siku ya NTDs na mafanikio ya “bilioni 12 kwa ajili ya dawa za NTDs” yaliyofanyika katika skuli hiyo , Wilaya ya Magharib ‘B’, Mkoa wa Mjini Mgahrib.
WAZIRI wa afya, Nassor Ahmed Mazurui akimpatia picha ya kuchora, Mwanamfalme wa Uingereza Sophie Helen, aliposhiriki maadhimisho ya siku ya NTDs na mafanikio ya “bilioni 12 kwa ajili ya dawa za NTDs” yaliyofanyika skuli ya msingi Kinuni A, Wilaya ya Magharib ‘B’, Mkoa wa Mjini Maghrib. (PICHA ZOTE NA FAUZIA MUSSA).
BAADHI ya wanafunzi wa Skuli ya Kinuni A wakifuatulia ufunguzi wa maadhimisho maadhimisho ya siku ya NTDs na mafanikio ya “bilioni 12 kwa ajili ya dawa za NTDs” yaliyofanyika skuli katika skuli hiyo iliyopo Wilaya ya Magharib ‘B’, Mkoa wa Mjini Magharib.
MSAMBAZAJI wa dawa za kutibu magonjwa yasiopewa kipaumbele ya NTDs ,Seif Bakar Shwaib akielezea hali ya magonjwa hayo kwa upande wa Zanzibar katika maadhimisho ya siku ya NTDs na mafanikio ya “bilioni 12 kwa ajili ya dawa za NTDs” yaliyofanyika skuli ya msingi Kinuni A, Wilaya ya Magharib ‘B’, Mkoa wa Mjini Magharib.

NA FAUZIA MUSSA

WAZIRI wa Afya Nassor Ahmed Mazrui, amesema Serikali ya MAPINDUZI YA Zanzibar inaendelea kuchukua hatua za ziada ili kupunguza maradhi yasiopewa kipaumbele Nchini ikiwemo matende, kichocho, minyoo na vikope.

Hatua hizo ni pamoja na kuondoa mazingira machafu, usimamizi mzuri wa Maji na kutunza usafi wa mazingira, pamoja na kuimarisha afya ya jamii.

Waziri Mazrui aliyasema hayo katika maadhimisho ya siku ya NTDs na mafanikio ya “bilioni 12 kwa ajili ya dawa za NTDs” yaliyofanyika skuli ya msingi Kinuni A, Wilaya ya Magharib ‘B’, Mkoa wa Mjini Mgahribi, na kuhudhuriwa na Mwanamfalme wa Uingereza Sophie Helen.

Alisema kutokana na uzowefu kuonenesha kuwa sehemu kubwa ya ugonjwa huo unapatikana Barani Afrika, Serikali kwa kushirikiana na wadau itaendelea kuchua jitihada za kupambana na ugonjwa huo ili kuhakikisha unamalizika nchini.

Alieleza kuwa Wizara ya Afya Zanzibar kupitia Kitengo cha Maradhi yasiyopewa kipaumbe (NTDs Program) itaendelea kutoa dawa za minyoo, kichocho na matende, kufanya ufuatiliaji wa walioathiriwa na magojwa hayo pamoja kuendeleza jitihada mbali mbali za kutoa matibabu ikiwa ni pamoja na matibabu ya chemotherapy ili kuyafikia malengo ya Shirika la Afya Duniani (WHO) juu ya kutokomeza magonjwa hayo ifikapo mwaka 2030.

Alisema takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya watu bilioni 1.5 wanadhaniwa kuambukizwa NTDs duniani kote ambapo waathirika zaidi wa magonjwa hayo ni kutoka katika nchi maskini zenye uhaba wa rasilimali.

Mazrui alisema katika kipindi cha Julai 2023 hadi Machi 2024, jumla ya watu 878 (Unguja 576 na Pemba 302) walichunguzwa maradhi ya kichocho katika hospitali na vituo vya afya, kati ya hao 731 (Unguja 445 na Pemba 286) waligundulika na maradhi hayo.

Alisema kati ya watu 79 waliochunguzwa maradhi ya matende katika kipindi hicho 33 waligundulika na vimelea vya ugonjwa huo na kupatiwa matibabu stahiki.

Mwanamfalme wa Uingereza Sophie Helen, ameipongeza Zanzibar kwa hatua iliyofikia ya kudhibiti ugonjwa wa Trakoma kwa kiasi kikubwa hali iliyopelekea kufikia mapema malengo yaliyowekwa na Jumuiya ya Madola (Commonwealth) ya kumaliza ugonjwa huo ifikapo mwaka 2030.

Mbali na hayo aliishukuru Serikali na uongozi wa Skuli ya Kinuni kwa ukaribisho wao hali iliyoonesha ukarimu wa wananchi wa Zanzibar, na kuahidi kuendelea kuisaidia Zanzibar ili kufanikiwa kumaliza magonjwa hayo.

Naye Mwakilishi wa Shirika la Afya la Duniani (WHO), Dk. Andemichael Ghirmay, alisema, shirika hilo limekuwa likitekeleza afua za kutokomeza magonjwa hayo ikiwemo kutoa elimu kwa wananchi na hata kuwezesha utumiaji wa dawa.

Hivyo, Dk. Ghirmay, aliwataka wadau wa sekta ya afya kuungana kwa pamoja na kushirikiana na WHO ili kusaidia kutokomeza magonjwa yasiyopewa kipaumbele.

“Magonjwa haya yana waathiri sana, hivyo WHO itahakikisha linashirikiana na Serikali ya Zanzibar kuhakikisha tunatokomeza haya magonjwa".

Msambazaji wa dawa za NTDs katika jamii Seif Bakar Shwaib alisema ni miaka 18 tangu kuanza kusambaza dawa hizo na kufanikiwa kuifikia asilimia 99 ya jamii ya Wazanzibar.

Mbali na mafanikio hayo msambazaji huyo alisema wakati wa zoezi la ugawaji wa dawa walikabiliwa na changamoto ya jamii kutokufahamu umuhimu wa dawa hizo hivyo kuwa na imani potofu, hali ambayo aliitaja kuzorotesha utendaji wao.

Hata hivyo wanaendelea kutoa elimu ya maradhi hayo na umuhimu wa kutumia dawa hizo ili iwasaidie katika utendaji kazi wao.

Kwa upande wake Naibu Mkurugrnzi Idara ya Kinga Wizara ya Afya Zanzibar Fatma Mohammed Kabole alisema maradhi hayo yanaathiri sana watu wenye hali duni, ambapo kwa Zanzibar maradhi ya vikope, kichocho, matende na minyoo yanaongoza kuathiri.

“miaka ya 86 magonjwa haya yaliathiri jamii kwa asilimia 80, kupitia mradi wakutokomeza magonjwa haya imepunguza idadi ya waathirika hadi kufikia asilimia 3 ya kichocho, na matende kuwa chini ya asilimia moja.” Alisema kabole

Alifahamisha kuwa maradhi ya kikope yaliathiri sana Mkoa wa Kaskazini Unguja na Micheweni Pemba ambapo magonjwa hayo yalichukua asilimia 11, kufuatia kugawa dawa na kuweka mikakati maalum ya kudhibiti ugonjwa huo maradhi hayo yamepungua na kuwa chini ya asilimia mbili.

Aidha alisema maradhi yanayosumbua sana kwa miaka hii ni minyoo kutokana na jamii kutochukua tahadhari za kujilinda na ugonjwa huo.

Kabole aliishauri jamii kuendelea kujikinga na maradhi hayo kwa kunawa mikono kabla ya kula hasa kwa watoto kwani ndio waathirika zaidi wa kichocho kuliko watu wazima.

Princess Sophie (Duchess of Edinburgh) ambae ni mke wa mtoto wa mwisho wa aliyekuwa Malkia wa Uingereza, Elizabeth II, Prince Edward, ambaye ni mdogo wa Mfalme wa sasa wa Uingereza, Charles III, yupo Zanzibar kwa ziara ya siku sita kutembelea miradi mbalimbali ya Afya inayotekelezwa na taasisi tofauti ambazo yeye ni mlezi wa miradi hiyo.

No comments: