Friday, October 25, 2024

PINDA AKUTANA NA RAIS WA BOTSWANA

 

Mkuu wa Misheni ya Uangalizi ya Uchaguzi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC - SEOM) kwenye Uchaguzi Mkuu wa Botswana na Waziri Mkuu wa zamani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Botswana Mheshimiwa Mokgweetsi Eric Keabetswe Masisi alipofika Ofisini kwa Mheshimiwa Masisi kujitambaulisha na ujumbe wake tarehe 24 Oktoba, 2024. Mhe. Pinda na ujumbe wake wako nchini Botswana  kuangalia uchaguzi mkuu wa nchi hiyo uliopangwa kufanyika tarehe 30 Oktoba 2024
Mkuu wa Misheni ya Uangalizi ya Uchaguzi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC - SEOM) kwenye Uchaguzi Mkuu wa Botswana na Waziri Mkuu wa zamani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda akisaini kitabu cha wageni alipowasilikatika Ofisi za  Rais wa Jamhuri ya Botswana Mheshimiwa Mokgweetsi Eric Keabetswe Masisi kujitambaulisha na ujumbe wake tarehe 24 Oktoba, 2024 jijini Gaborone
Mkuu wa Misheni ya Uangalizi ya Uchaguzi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC - SEOM) kwenye Uchaguzi Mkuu wa Botswana na Waziri Mkuu wa zamani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda akizungumza na Rais wa Botswana, Mheshimiwa Mokgweetsi Eric Keabetswe Masisi (kushoto), alipokutana na ujumbe wa SEOM katika Ikulu ya Gaborone tarehe 24 Oktoba 2024. Kulia ni Katibu Mtendaji wa SADC, Mheshimiwa Elias Magosi.

Rais wa Jamhuri ya Botswana, Mheshimiwa Mokgweetsi Eric Keabetswe Masisi (kushoto) akizungumza na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi ya Uchaguzi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC - SEOM) kwenye Uchaguzi Mkuu wa Botswana na Waziri Mkuu wa zamani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda alipokutana na ujumbe wa SEOM katika Ikulu ya Gaborone tarehe 24 Oktoba 2024. Kulia ni Katibu Mtendaji wa SADC, Mheshimiwa Elias Magosi.

Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC-SEOM), Mheshimiwa Mizengo Pinda, amekutana na Rais wa Jamhuri ya Botswana, Mheshimiwa Mokgweetsi Eric Keabetswe Masisi, katika ofisi yake jijini Gaborone. SEOM ilitumia ziara hiyo kujitambulisha kwa Mhe. Rais Masisi na kubadilishana mawazo kuhusu hali ya kidemokrasia na maendeleo nchini Botswana. 

Akizungumza na Mheshimiwa Masisi, Mheshimiwa Pinda alisisitiza wajibu wa SEOM kulingana na Misingi na Mwongozo wa SADC kuhusu Uchaguzi wa Kidemokrasia na kuonesha utayari kwa SEOM kutekeleza jukumu la uangalizi katika uchaguzi mkuu ujao wa Botswana.

Mhe. Pinda alieleza shukrani zake kwa mapokezi mazuri aliyoyapata yeye na timu yake tangu walipowasili Botswana na kumueleza Mhe. Rais Masisi kuwa kabla ya kukutana na yeye, SEOM ilikutana na kuzungumza na wadau mbalimbali, ambao ni pamoja na Tume Huru ya Uchaguzi ya Botswana (IEC), Kamishna wa Polisi wa Botswana, Wizara ya Mambo ya Nje, viongozi wa vyama vya kisiasa, NGO, na Mabalozi wanaowakilisha Botswana na SADC. 

Aliongeza kuwa timu hiyo pia ilipitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii ili kupata ufahamu kuhusu masuala yanayohusiana na uchaguzi mkuu ujao wa nchi hiyo.

Kwa upande wake, Mhe. Rais Masisi aliwakaribisha waangalizi wa SEOM na kuwahakikishia kuwa Batswana iko tayari kwa uchaguzi mkuu utakaofanyika tarehe 30 Oktoba 2024 na kuongeza kuwa Serikali ya Botswana iko tayari kushirikiana na wadau wote, ikiwa ni pamoja na waangalizi na aliwaambia SEOM kuzungumza na yeyote wanayefikiri atawasaidia kutekeleza jukumu lao la uangalizi.

“Serikali iko tayari kufanya kazi na waangalizi; nendeni mkazungumze na yeyote mnayefikiri anaweza kuwasaidia nyinyi na timu yenu kufanya kazi zenu vizuri. Botswana ni nyumbani kwa SADC; nyote mnakaribishwa hapa na fanyeni kazi yenu  kwa uhuru," alisisitiza Mheshimiwa Masisi.

Alisema anaamini kuwa Tume Huru ya Uchaguzi ya Botswana (IEC) imeshirikisha wadau wote wanaohusika na uchaguzi huo mkuu, na kwamba Serikali yake ina imani kuwa kila kitu kitakuwa sawa na uchaguzi utakuwa huru, haki, na wa kuaminika, na kwamba usalama na amani vitakuwepo wakati wa uchaguzi na hata baada ya uchaguzi huo.

Aliwahakikishia wajumbe wa SEOM kuwa Serikali imetumia rasilimali zote zilizopo kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa mafanikio makubwa na alisisitiza kuwa Serikali iko tayari kutoa msaada wowote kwa SEOM pale itakapohitajika.

Septemba 2024, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa Ulinzi na Usalama ya  SADC TROIKA, alimteua Mheshimiwa Pinda kuongoza Misheni ya  Uangalizi wa SADC katika uchaguzi mkuu wa Botswana.

SEOM ilijumuisha maafisa kutoka Sekretarieti ya SADC, wanachama wa Taasisi ya SADC Troika kutoka Jamhuri ya Malawi, Zambia, na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na Baraza la Ushauri la Uchaguzi la SADC (SEAC).


No comments: