Advertisements

Saturday, December 13, 2014

MBUNGE CCM ASIMULIA ALIVYOPOFUKA MACHO!


Dk. Mpanda na mkewe wakisalimiana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda wakati akiwa Mbunge.

Stori: Deogratius Mongela na Chande Abdallah
Ni stori ya kusikitisha sana! Aliyekuwa Mbunge wa Kilwa Kaskazini mkoani Lindi kwa ‘leseni’ ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kati ya mwaka 2005 hadi 2010, Dk. Samson Mpanda, amesimulia jinsi alivyopata upofu akiwa kwenye nafasi yake ya ubunge, tatizo ambalo lilimuanza mwaka mmoja tu baada ya kuchaguliwa na kuanza kuhudhuria vikao vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mjini Dodoma.

Akisimulia mkasa huo wa kuumiza mbele ya waumini wa Kanisa la The Revelation Church chini ya Nabii Yaspi Bendera lililopo Buza-Kipera jijini Dar, Dk. Mpanda aliyeongozana na Diwani wa Kata ya Kijichi, William Ntiwundi ambaye ni kaka yake, alidai kwamba alifika kanisani hapo baada ya kuuguza macho yake katika hospitali mbalimbali bila mafanikio.

Mbunge huyo ambaye kwa sasa anashinda kwenye maombi alieleza kuwa, kabla ya kugombea nafasi hiyo hakuwa na matatizo yoyote ya macho lakini alipotangaza tu kupitia kura za maoni ndipo tatizo lilipoanza.

Dk. Mpanda alisema kuwa alishinda kiti hicho mwaka 2005 na kuanza shughuli za kulitumikia jimbo lake lakini mwaka mmoja baadaye alijikuta akipofuka macho na kushindwa kuona jambo lililomfanya aanze kutafuta tiba ambapo tatizo lake halikutatuliwa na madaktari wakidai kuwa hawezi kuona tena.

Alieleza kwa masikitiko kwamba ulipofika uchaguzi mwingine ilibidi aachie ngazi ambapo nafasi yake ilichukuliwa na Multaza Mangungu (Mbunge-CCM) anayeitumikia hadi sasa.

“Baada ya kupata hali hii nilikumbuka vitisho nilivyokuwa nikivipata wakati wa kugombea na wakati niliposhinda, nikagundua kuwa vitisho hivyo vilikuwa na mambo ya kishirikina ndani yake,” alisema Dk. Mpanda na kusababisha huzuni kubwa kanisani hapo.

Wanahabari wetu walishuhudia tukio la mbunge huyo akiombewa na Nabii Yasip ambaye alisema kuwa Dk. Mpanda alifanywa kipofu kutokana na roho mbaya za watu huku akiahidi kumuombea na hatimaye kurudia hali yake.

GPL

No comments: