Advertisements

Friday, July 31, 2015

Kwanini naunga mkono kwa Mh Edward Lowassa kukaribishwa UKAWA : Ismail Jussa

Mjadala mkubwa umezuka kuhusu mwelekeo wa ushirikiano wa vyama vikuu vya upinzani vinavyounda UKAWA na hatua ya kumkaribisha Waziri Mkuu mstaafu na Mbunge wa Monduli, Mhe. Edward Lowassa, ili kushirikiana kuiondosha madarakani CCM pamoja na mfumo wake wa kikandamizaji na kifisadi ulioambatana na kiburi kikubwa cha watawala.

Baada ya kusoma maoni na mitazamo ya watu mbali mbali, nataka na miye nieleze mtazamo wangu kuhusiana na masuala hayo lakini zaidi nikirudi nyuma katika miaka ya 1991 na 1992 ambapo kulikuwa na vuguvugu zito la kudai mabadiliko ya mfumo wa utawala katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hasa baada ya kuangushwa Ukuta wa Berlin na kuporomoka kwa dola kandamizi za kikomunisti na washirika wao zilizokuwa zikijitambulisha na Kambi ya Mashariki zama za Vita Baridi (Cold War). Tanzania haikusalimika. Na mimi nikiwa kijana mdogo wa miaka 19 nilikuwa katikati ya vuguvugu hilo.

Sote tunajua kwamba demokrasia ya vyama vingi inastawi pale nchi inapokuwa na uwanja wa ushidani ulio sawa (level playing field).

Mwaka 1991, Tume ya Jaji Francis Nyalali iliyopendekeza kurudishwa kwa mfumo wa demokrasia ya vyama vingi ilipendekeza pia, kupitia Taarifa yake iliyokuwa na vitabu (volumes) vitatu, haja ya kwanza kubadilisha Katiba, Sheria na misingi ya Utawala katika maeneo mengi ili kuondoa nafasi ya CCM kudhibiti hatamu zote na pia kudhibiti taasisi zote kuu za nchi pamoja na rasilimali nyingi ambazo kimsingi zilipatikana kupitia michango ya lazima iliyokamuliwa kwa wananchi ambao wengi wao hawakuwa hata wanachama wa CCM.

Kwa mukhtasari ni kwamba Tume ya Nyalali ilitaka kwanza CCM kiondolewe nguvu hizo kubwa ambazo haikuzipata kutokana na kazi ya kisiasa iliyofanya au kukubaliwa kwake kwa hiyari na wananchi bali kutokana na kuhodhi kwake kwa mabavu mamlaka makubwa chini ya dhana ya "Chama kushika hatamu" (Party Supremacy), dhana iliyokifanya kisiwe chama cha siasa bali ni chama dola (state party) ambacho kilikuwa siyo tu chama pekee cha siasa lakini zaidi ilikiweka juu ya mamlaka na taasisi nyengine zote za dola tena kwa mujibu wa Katiba na Sheria za Nchi.

Kwa kutumia dhana hiyo ya "Chama kushika hatamu" (Party Supremacy), Katiba na Sheria za Nchi ziliiweka CCM kuwa juu ya Serikali, Bunge, Mahkama na hata Vyombo vya Ulinzi na Usalama. Tume ya Nyalali kwa usahihi kabisa iliona hali hiyo itaondoa kabisa dhana nzima na maana ya kuruhusu demokrasia ya vyama vingi nchini na itapelekea CCM kuwa juu ya vyama vingine si kwa sababu ya kukubalika kwake na wananchi bali kwa sababu ya mfumo wa kikatiba, kisheria na Utawala unaokilinda.

Kwa sababu hizo, ndiyo Tume hiyo iliyoongozwa na Jaji aliyeheshimika sana Francis Nyalali ikaja na mapendekezo mengi ya hatua ambazo kama zingetekelezwa zingeuweka uwanja sawa wa ushidani kwa vyama vyote vya siasa. 

Tume hiyo ilikuja na mapendekezo ya ratiba kamili ya utekelezaji wa hatua hizo. Lakini kwa sababu CCM ilijua kuwepo kwa ushidani ulio sawa kutakipa wakati mgumu kushindana na vyama vipya ILIYAKATAA mapendekezo hayo yote. Hiyo ndiyo hali tunayoendelea nayo hadi leo.

Hali ya namna hiyo haikuwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tu bali ndivyo ilivyokuwa kwa nchi takriban zote za Afrika ambazo kwa miaka mingi tokea Uhuru zilikuwa na tawala za chama kimoja vilivyohodhi mamlaka zote za nchi.

Katika hali kama hiyo, kuwa na uchaguzi huru na wa haki linakuwa ni jambo gumu na kukishinda chama dola (state party) kuwa takriban jambo lisilowezekena.

Njia pekee inayobaki ya kuweza kujenga mfumo imara wa ushindani huru na wa haki ndani ya demokrasia ya vyama vingi katika nchi kama hizo ni kwanza kuhakikisha kuwa chama dola (state party) kinaondolewa madarakani ili kutoa nafasi ya ujenzi wa mfumo mpya wa demokrasia iliyojengwa juu ya misingi imara ya haki na inayorudisha mamlaka ya kuendesha nchi na hatamu zake kwa wananchi wenyewe.

Ili kufikia hapo, uzoefu wa nchi nyingi umeonesha kwamba hatua mbili ni lazima zifanyike. Kwanza, vyama vya upinzani viunganishe nguvu zake; na pili, chama dola kigawike. 

Hatua hizo ndizo zilizoving'oa vyama vya KANU nchini Kenya, UNIP na hata MMD nchini Zambia pamoja na MCP nchini Malawi. Hata Zimbabwe katika uchaguzi wa mwanzo ambao ulikipa ushindi MDC dhidi ya ZANU-PF cha Robert Mugabe, hali ilikuwa hivyo hivyo kabla ya Mugabe kuamua kuitia nchi katika machafuko makubwa ili aendelee kubaki madarakani. Mfano wa karibuni kabisa ni wa Nigeria pale chama cha APC cha Rais Muhammad Buhari kilipofanikiwa kukin'goa chama cha PDP cha Goodluck Jonathan na watangulizi wake. Tukio la Olesagun Obasanjo kuchana kadi yake ya PDP ndiyo iliyohitimisha safari ya chama hicho kuondoka madarakani.

Ni katika muktadha huo, naona kwamba njia pekee ya kukiondoa madarakani CCM na mfumo wake dhalimu na kandamizi, ambao ndiyo unaolea ufisadi na rushwa, kuua uwajibikaji hapa nchini na hatimaye kuwaingiza Watanzania katika umasikini wa kutupwa wakati nchi yenyewe imejaa utajiri wa kila aina, ni kuunganisha nguvu za vyama vya upinzani na kugawanyika kwa CCM yenyewe.

Kuundwa kwa UKAWA na sasa kupasuka kwa CCM kwa hatua ya Mhe. Edward Lowassa na kundi kubwa linalomuunga mkono ndani ya chama hicho kukihama na kujiunga na UKAWA ni fursa ya kihistoria ambayo tunapaswa kuikumbatia ili CCM ifuate mkondo wa vyama dola vyengine vya Afrika na kuipa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nafasi ya kupata MWANZO MPYA utakaotukwamua katika mkwamo huu tuliokwamishwa na CCM.

Viongozi wakuu na wakongwe wa siasa za CCM wanapoliona ANGUKO LA CCM tujue sasa zama zake zimefikia kikomo na TANZANIA MPYA INAKARIBIA KUZALIWA.

* Karibu Edward Lowassa
* Ahsante UKAWA

6 comments:

Unknown said...

Umeshindwa kutambua kwamba nini CCM ndiyo iliyoruhusu mfumo wa vyama vingi licha ya watanzania walio wengi kuukataa
Ukawa hauta tuletea mabadiliwa ya kweli maana unaundwa na Lowassa pamoja na mtandao wake wa kifisadi kutoka CCM

Anonymous said...

Ni aibu, muungano wa vyama vyenye slogan "Peoples power" baada ya miaka 23, tangu (1992), bado Vyama hivi vinategemea mamluki, wako wapi wagombea wenye uwezo wa kuwaongoza Watanzania na wenye msimamo mbadala wa chama cha mapinduzi. Napenda kumnukuu Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius K. Nyerere,“Watanzania wanahitaji mabadiliko na wasipoyapata ndani ya CCM watayafuata nje ya CCM”. Nitauamini vipi upande wa nje ya CCM kama viongozi wanaosimamia nje ya CCM hawakuuona ubaya wa CCM mpaka waliposukumiwa nje, Kama kweli viongozi hawa wangekuwa na imani hii wangetangaza asubuhi na mapema kama alivyofanya Lembeli. Mimi Binafsi bado naamini kauli ya baba wa Taifa, naomba kunukuu, “Rais wa Tanzania anaweza kutoka Chama cho chote kile, lakini Rais bora wa nchi yetu atatoka CCM!

Anonymous said...

Ndugu jussa huo ukuta wa Berlin au kama ulivyojulikana na wajurumani wenyewe (Berliner mauer) unahusiana na nini na siasa za kwetu?
Hiyo cold war unayoizungumzia ndio iliyoibua China na mfumo wake wa chama kimoja, kwa sasa China ni taifa lenye nguvu linaloogopewa na mataaifa makubwa yanayojiita ya kidemokrasia. China ni nchi yenye kufuata mfumo wa chama kimoja na ni mfumo uliyowavusha kwa maendeleo ya kasi ya ajabu.
Kwa hiyo msitake kutudanganya hapa kuwa watu wa vyama vya upizani au vyama vingi ndio suluhisho pekee ya matatizo ya watanzania. Kuna ushahidi tosha kuwa hivyo vyama vingi ndivyo vitakavyoiangamiza Tanzania na kuitia katika matatizo makubwa kabisa. Kama kenya wapinzani walishawahi kushika hatamu kipi cha kujivunia wakati ukabila umekithiri, ardhi karibu yote inamilikiwa na wageni tena ile yenye rutuba.
Mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yameshaharimu maisha ya watu wengi kiwango cha kusikitisha. Ukiacha kenya nchi gani africa watu vyama vingi walio leta maendeleo ya kweli.
Zambiani chiluba na chama chake wazambia walikuwa wanataka mabadiliko ya kweli wakamueleza mzee kaunda kwa kura kwamba wanataka mabadiliko kwa kutokichagua chama chake na kuwakabidhi wapinzani wakiongozwa na chiluba kilichotokea wazambia hawatasahu maishani mwao.
Seif Sharif, Ibrahim lipumba, Dk slaa, Eduwadi lowasa na wengi viongozi wa vyama vya upizani Tanzania hawana tofauti na Raisi wa Burundi ni waroho wa madaraka wapo tayari watu wapoteze maisha yao wakiamini kuwa wao pekee ndio wenye haki ya kuingia ikulu. Kwani unafikiria CUF Zanzibar ndani ya cuf hakuna watu wenye uwezo wa kugombea uraisi isipokuwa seif Sharif, Niamini wapo tena wengi na wanamzidi kitaaluma na kila Kitu lakini jamaa ni dikteta ndani ya chama vipi leo aaminiwe kupewa nchi? halikadhalika kwa lipumba ninaamini wapo watu wengi tu wenye uwezo zaidi yake kwa nini miaka nenda miaka rudi ya uchaguzi anganganie kutaka kuchaguliwa kuwa raisi halikadhalika dk slaa vilevile. Sasa lowasa juu ya hao wote kwa uchu wa madaraka,wasi wasi wangu hata atakapo kuja kushindwa kihalali kabisa katika uchaguzi mkuu kutakuwa kuna kazi katika nafsi yake na watu wake wanaomsapoti kukubaliana na matokeo. Usiku au mchana lowasa na ukawa hawamuwezi magufuli. Watazania waposmart hivi sasa uchaguzi unaokuja watu katika tiketi ya uraisi hawatakwenda kupiga kura kuhusu chama gani bali mtu gani na kwa hilo simuoni lowasa anaweza kusimama na magufuli. CCM wamesoma katika chaguzi zilizopita baada ya kupoteza majimbo ambayo hawakuwapeleka wagombea waliopendekezwa na wanachi. Na kwa kila hali magufuli ni chaguo sahihi la watanzania dhidi ya lowasa. Hata katika upizani lowasa ni chaguo la viongozi sio la wananchi. Wananchi hawamtaki lowasa na kweli hiisio demokrasia kuwateulia mtu aliejaa kashfa za ufisadi.

Anonymous said...

CC M haina mamlaka yakuruhusu vya ma vingi wananchi ndio Wali taka kuwepo mfumo wa vya ma vingi. Huwezi kusema CCM ndio waliruhusu kana kwamba wao ndio owners wa nchi.

Anonymous said...

Ni kweli mwaka 1992 ilipigwa kura Ya maoni na wananchi wakasema chama kimoja kiendelee kwa 92% na 8% wakasema vyama vingi. Kwa busara ya ccm wakasema hiyo 8% pia ni watanzania mfumo wa vyama vingi uruhuaiwe. Sasa huyu jussa hata hujui historia na anaingiza mambo ya ujerumani magharibi na mashariki kwa siasa ya tanzania!!! Kweli mabilioni ya lowasa yameshawakaanga akili. Hiyo ndiyo ukawa hata historia ya nchi hawajui

Anonymous said...

Hongera jusa , uliyozungumza ni sahihi, waache watape tape kwa kutumia hoja ya nguvu,hao hawajui historia ,wape darasa.........