Baada ya kuenea kwa uvumi kuwa Naibu Katiba Mkuu wa Chadema, John
Mnyika anataka kuachana na chama hicho, kiongozi huyo ameibuka na
kukanusha akisema: “Hakuna kitu kama hicho na wala sina mpango wa
kuhama.”
Mnyika alisema hayo jana alipopigiwa simu ili azungumzie
taarifa hizo. Mbunge huyo wa Kibamba alisisitiza kwamba huo ni uzushi.
Habari za kujiuzulu kwa Mnyika zilianza kusambaa katika vyombo vya
habari kwa mara ya kwanza mwaka 2013 baada ya aliyekuwa naibu katibu
mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe kufukuzwa uanachama.
Wakati huo, uvumi
ulienea kwenye mitando kwamba amejivua nyadhifa zake zote na kwamba
ameshakabidhi barua yake kwa katibu mkuu wakati huo, Dk Willibrod Slaa.
Habari hizo zilijirudia mara baada ya Dk Slaa kutangaza kujivua nyadhifa
zake zote ndani ya chama hicho huku akipinga hatua yake ya kumtangaza
Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kuwa mgombea wake wa nafasi ya
urais.
Licha ya kushindwa kujitokeza hadharani kukanusha wala
kuthibitisha tetesi hizo, Mnyika alionekana kuendelea na shughuli zake
za kisiasa kama kawaida.
Uvumi wa tatu
uliibuka mwishoni mwa wiki iliyopita safari hii ilidaiwa kueleza msimamo
wake kuhusu Lowassa kupitishwa na Chadema na kisha Ukawa kuwania urais
ikidaiwa kwamba anataka kiongozi huyo ahojiwe na kuchukuliwa hatua
kutokana na ushiriki wake katika kashfa ya Richmond.
Habari hiyo
iliyoibua hisia za wengi ilimnukuu Mnyika akisema: “Msimamo wangu
haujabadilika kama ambavyo niliwahi kusema nikiwa mkurugenzi wa vijana
wa Chadema tarehe 25 Februari 2008 na kipindi chote nikiwa Mbunge wa
Ubungo…. Hivyo nategemea kuanzishwa kwa Mahakama ya Mafisadi Lowassa
ndiye atakuwa wa kwanza. Siwezi kusaliti msimamo wangu bora nipoteze
ubunge wangu.”
Katika mwendelezo wake, baadaye uvumi mwingine uliibuka
kwamba baadhi ya viongozi wa chama hicho walionekana nyumbani kwa Mnyika
wakimsihi asichukue uamuzi huo.
Hata hivyo, hakuna kiongozi yeyote wa
Chadema aliyewahi kuzungumzia suala hilo kabla ya hivi karibuni, Ofisa
Habari Mwandamizi wa Chadema, Tumaini Makene kutoa taarifa ya kukanusha
akisema huo ni mradi wa kutengeneza uongo unaofadhiliwa na watu kwa
ajili ya kukisumbua chama na Watanzania akisema wakati habari hizo
zinaenezwa, Mnyika alikuwa akifanya shughuli za chama.
No comments:
Post a Comment