Advertisements

Tuesday, June 6, 2017

Wanaodaiwa kunywesha mtu dawa za kulevya watiwa mbaroni

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Urich Matei.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro linawashikilia watu watatu wanaodaiwa kuwa vinara wa kuwawekea watu dawa za kulevya kwenye vinywaji na vyakula katika vyombo vya usafiri.

Kamanda wa Polisi Mkoani hapa, Urich Matei alisema kuwa tukio hilo ni la Novemba 13 mwaka jana katika maeneo ya Chalinze na Morogoro katika moja ya basi la abiria, lililokuwa likitokea Morogoro kwenda Dar es Salaam.

Alitaja watuhumiwa hao kuwa ni Sudi Rutahiwa (32), mkazi wa Mbagala Maji Matitu jijini Dar es Salaam, Aston Kamala(28) mkazi wa Kitunda Mzinga Dar es salaam na Mugisha Filbet (40), mkazi wa Kibaha mkoani Pwani.

Kwa mujibu wa kamanda Matei, watuhumiwa hao walimpa juisi abiria mmoja ambayo ilichanganywa na dawa za usingizi aina ya Lorivan-2 inayotumika katika hospitali kwa wagonjwa wenye matatizo ya akili kisha wakamuibia simu tatu, komputa ndogo (laptop) moja na Sh.700,000.

Kwa upande wake, abiria anayedaiwa kuwekewa dawa hizo akiwa katika basi hilo, Angaza Gimbi ambaye ni mkazi wa Morogoro anayefanya kazi jijini Dar es Salaam, alisema kuwa siku hiyo alikuwa anasafiri na basi kuelekea Dar es Salaam na alikaa na mtu kwenye siti ambaye alikuwa upande wa dirishani, lakini baada ya muda yule mtu akamuomba ahamie alipokuwa amekaa yeye, kwa madai ya kuwa na matatizo.

Alidai baada ya kuhamia dirishani na kukaa kwa muda kidogo, yule mtu akamwambia afungue dirisha, ambapo alifungua dirisha. Lakini, baada ya muda kidogo yule mtu akaamua kufungua zaidi yeye mwenyewe lile dirisha.

Baada ya tukio hilo, hakuelewa tena chochote mpaka alipopata fahamu akiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili. Alilishukuru jeshi la polisi mkoa wa Morogoro kwa ushirikiano wao hadi kufanikisha kupatikana kwa watuhumiwa hao.

HABARI LEO

No comments: