Advertisements

Tuesday, October 10, 2017

MUGABE AFANYA MAAMUZI MAGUMU KAMA YA RAIS MAGUFULI

Rais Robert Mugabe.

HARARE, ZIMBABWE: Ikiwa ni siku tatu baada Rais John Magufuli kufanya mabadiliko ya Baraza lake la Mawaziri hapa nchini, Rais Robert Mugabe amefanya mabadiliko katika Baraza la Mawaziri ambalo amewaondoa baadhi na kuingiza sura mpya lakini habari kubwa ni kushushwa kwa makamu wa rais wake, Emerson Mangagwa.

Katika mabadiliko hayo, Mangagwa sasa atakuwa waziri wa utalii hali ambayo imetafsiriwa kwamba ameshushwa cheo.

Shirika la habari la ZimNews, likinukuu chanzo cha uhakika kutoka ndani ya serikali limesema Mnangagwa alikwishadokezwa kujiandaa kwa makubwa yanayotarajia kumfika na sasa amepokonywa nafasi zote za makamu wa rais na ile ya makamu wa rais katika chama tawala cha Zanu-PF.

Wakati fulani Mnangagwa alikuwa anapewa nafasi ya kumrithi Mugabe ikiwa atafariki dunia au kuamua kung’atuka. Lakini katika siku za hivi karibuni alianza kutopikika na wenzake hususan mke wa Raus Mugabe, Grace Mugabe.

Mnangagwa aliwahi kushutumiwa na mwanamama huyo kwamba anashirikiana na watu waliofukuzwa Zanu PF. Pia, alishutumiwa na Grace kuwa alikuwa anafanya njama za kutaka kumpindua rais ili arithi nafasi yake.

Kilichomponza zaidi ni king’ang’anizi chake kwamba alikula sumu iliyokuwemo kwenye Ice Cream kutoka kampuni ya maziwa inayomilikiwa na Grace na akapelekwa Afrika Kusini kwa matibabu. Rais Mugabe alisema aliambiwa na madaktari waliokuwa wanamtibu makamu huyo wa rais kwamba kuugua kwake hakukutokana na sumu, lakini yeye alishikilia kwamba alilishwa sumu hali iliyoonekana ni kumdhalilisha Rais Mugabe.

Haya yakiwa hivyo, ndani ya Zanu PF kuna makundi makubwa mawili yanayonyukana kuwania uteuzi wa kugombea urais; la kwanza linaitwa G40 ambalo kuna makamu wa Rais Phelekezela Mphoko huku likiungwa mkono na Grace, na la pili linaitwa Lacoste ambalo linaongozwa na Mnangagwa. Kwa mabadiliko haya ni kama makamu huyo wa rais amepunguzwa kasi.

Aliyekuwa Waziri wa Fedha Patrick Chinamasa nafasi yake imechukuliwa na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani Ignatius Chombo, ambaye ni katibu mkuu wa Zanu PF anayehusika na masuala ya utawala. Wadadisi wa masuala ya siasa wameshtushwa na uteuzi huo wakihoji atafanya nini kuhusu sarafu ya Zimbabwe ambayo inaendelea kushuka.

Chinamasa amepewa wizara mpya isiyofahamika ya Usalama wa Mitandao. Muda mfupi baada ya kupewa nafasi hiyo, mwigizaji maarufu Carl Joshua Ncube alitania: “Jamani Patrick Chinamasa anawafuatilia kwenye Twitter “.

Aliyekuwa Waziri wa Utalii, Walter Mzembi sasa ameteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje.

Mpwa wa Mugabe, Patrick Zhuwao anayeonekana kuwa mfuasi mkuu wa kundi la G40 linalopigiwa upatu na Grace ameteuliwa kuwa Waziri wa Kazi akitokea Wizara ya Vijana na Utamaduni.

Hatua ya kupandikwa kwake ni ushahidi wa kutosha kwamba umelenga kulipa nguvu kundi la G40 dhidi ya lile la Mnangagwa linaloitwa Lacoste.

GPL

No comments: