Advertisements

Monday, December 25, 2017

MAAMUZI YA TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI KUHUSU RUFAA MOJA YA MGOMBEA UBUNGE NA RUFAA MBILI ZA WAGOMBEA UDIWANI

Kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 40(6) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343 ikisomwa pamoja na Kanuni za 34 na 35 za Kanuni za Uchaguzi wa Rais na Wabunge za mwaka 2015, Tume ilipokea Rufaa moja kutoka kwa Mgombea wa Ubunge jimbo la Singida Kaskazini kwa tiketi ya Chama cha AFP akipinga maamuzi ya Msimamizi wa Uchaguzi ngazi ya Jimbo dhidi ya pingamizi alilomuwekea Mgombea wa CCM.
Aidha, kwa mujibu wa masharti ya kifungu cha 44 (5) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292 ikisomwa pamoja na Kanuni za 28 na 29 za Kanuni za Serikali za Mitaa (Uchaguzi wa Madiwani) za mwaka 2015, Tume ilipokea Rufaa mbili. Rufaa ya kwanza ilitoka kwa Mgombea wa Udiwani Kata Keza – Halmashauri ya Wilaya Ngara kwa tiketi ya CCM akipinga maamuzi ya Msimamizi  wa Uchaguzi ngazi ya Jimbo dhidi ya pingamizi alilomuwekea Mgombea wa NCCR - Mageuzi. Rufaa ya pili ilitoka kwa Mgombea wa Udiwani Kata ya Kwagunda – Halmashauri ya Wilaya Korogwe kwa tiketi ya CCM akipinga maamuzi ya Msimamizi wa Uchaguzi ngazi ya Jimbo dhidi ya pingamizi alilomuwekea Mgombea wa CUF.
Katika kikao chake cha kawaida kilichofanyika tarehe 24 Desemba, 2017 siku ya jumapili, Tume ilipitia Rufaa hizo na kuamua kama ifuatavyo:
Kuhusu Rufaa ya Mgombea Ubunge, Tume imekubaliana na maamuzi ya Msimamizi wa Uchaguzi na hivyo Mgombea aliyekatiwa Rufaa aendelee kuwa mgombea wa Ubunge Jimbo la Singida Kaskazini.
Kuhusu Rufaa za Wabombea Udiwani Kata ya Keza Halmashauri ya Wilaya ya Ngara na Kata ya Kwagunda – Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe, Tume imekubaliana na maamuzi ya Wasimamizi wa Uchaguzi na hivyo Wagombea Udiwani waliokatiwa Rufaa waendelee kuwa wagombea wa Udiwani katika Kata husika. 
Taarifa rasmi za maamuzi ya Tume zimetumwa kwa Wasimamizi wa Uchaguzi ili wawapatie wahusika maamuzi hayo.

Imetolewa leo tarehe 25 Desemba, 2017 na
Kailima, R.K
MKURUGENZI WA UCHAGUZI

No comments: