Advertisements

Tuesday, June 2, 2020

Mwanafunzi atengeneza barakoa na kuzigawa bure

Mwandishi Wetu, Mtanzanmia

Mwanafunzi wa shule ya sekondari mkoani Dar es Salaam, Rania Nasser ameunda kikundi cha kutengeneza barakoa bure kwa wahitaji ili kujikinga na virusi vya corona.

Kikundi hicho kinachojulikana kama Barakoa TZ lengo lake kubwa lilikuwa kutengeneza barakoa nyingi na kuzigawa bure kwenye vituo vya polisi vilivyo karibu na nyumbani kwao bure kabisa.

Rania anasema baada ya wiki moja ya kugawa barakoa hizo, uhitaji uliongezeka maradufu na hivyo akaona umuhimu wake ukiongezeka.

“Kwa sababu hiyo, ilinilazimu kuomba usaidizi kwa marafiki na ndugu zangu wa karibu ili kukabiliana na uhitaji wa barakoa.

“Kwa sasa zimepita wiki kadhaa tangu kuanzishwa kwa Kikundi cha Barakoa Tz na tayari tushatengeneza na kugawa zaidi ya barakoa 1,000 kwenye vituo vya watoto yatima, wahudumu wa afya, polisi lakini zaidi kwa wale wenye uhitaji.

“Hii imefanikiwa kutokana na kutumia muda mrefu kwenye kushona barakoa kutoka kwa wasamaria wema na wafadhili,” amesema Rania.

Rania kwa sasa anasema licha ya kuwa na baadhi ya wasamaria ambao wanashona barakoa mkoani Mwanza, Dodoma na Dar es Salaam pamoja na kusambaza mitaani mtaani lakini wanahitajika wengi zaidi.

“Naomba na wengine wajitokeze kusaidia hili jambo, hata kama huwezi kushona kwa haraka, hiyo haina shida ni sawa kwani barakoa moja inaweza kuokoa maisha ya watu wengi.,” amesema.

Kuhusu aina ya kitambaa cha kushonea, Rania amesema yeye hupata aina zote tofauti za mifumo na atachukua kitambaa cha aina yoyote ambacho anaweza kupata isipokuwa jambo moja la kuhakikisha kuwa ni cha pamba.

“Kitambaa cha kunyoosha kinaruhusu chembe zaidi kupita katikati ambayo si kile unachotaka kwa ajili ya kufunika uso,” amesema.

Pamoja na mambo mengine, Rania anasema kwa sasa anatengeneza barakoa nyingi kwa ajili ya watoto na anatoa wito kwa wenye miundo zaidi ya kitambaa cha watoto au mifumo mingine kushirikiana ili kuja na aina mbalimbali tofauti.

No comments: