Thursday, August 20, 2015

Ubora wanogesha Ngao ya Jamii

Yanga
Azam

Dar es Salaam. Ubora wa Azam na Yanga unalifanya pambano baina yao Jumamosi ligeuke gumzo mitaani kwa sasa.
Pambano hilo la Jumamosi la Ngao ya Jamii litakuwa mahususi kwa uzinduzi wa msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Timu hizo kila zinapokutana kwa sasa zimekuwa ni mechi inayoibua mambo kadhaa ya kufurahisha ndani na nje ya uwanja.
Kikubwa wiki hii ni kumbukumbu  ya timu  hizo zilipokutana kwenye robo fainali ya Kombe la Kagame ambako zilimaliza dakika 90 bila bao.
Tangu wakati huo, timu hizo mbili zimefanikiwa kujiandaa vya kutosha kuelekea pambano hilo.
Kinachofurahisha ni kwamba timu hizo zote zimecheza mechi tatu za kirafiki katika kambi zao na zote zimeshinda.
Azam ilianza kwa kuifunga KMKM bao 1-0 kisha  ikaichapa Mafunzo (3-0)  na mwisho ikaifunga  JKU ( 2-0).
Yanga ilianza kwa kuichapa Kimondo FC (4-1), ikaifunga Prisons ( 2-0) na  Mbeya City (3-2).
Hata hivyo, Azam inaonekana ina ukuta imara kuliko Yanga na hivyo kuzidi kuwapa wakati mgumu washambulaiji wa Yanga kuipenya ngome hiyo.
Kitakwimu, Azam haijaruhusu bao katika michezo mitatu ya kirafiki kisiwani Zanzibar kama ilivyokuwa kwenye Kombe la Kagame na hivyo kuendelea kuwa na safu ya ulinzi imara nchini.
Safu ya ushambuliaji ya Yanga imeonekana tishio kwenye michezo hiyo ya kirafiki kwani katika mechi tatu  imefunga mabao tisa, lakini ikionekana bado kuna kazi katika safu ya ulinzi ya timu hiyo kwani imeruhusu mabao matatu.
Safu hiyo hivi sasa inaundwa nao, Kelvin Yondani,  beki mpya  raia wa Togo, Vincent Bossou badala ya Nadir Haroub ‘Cannavaro’ anayesumbuliwa na malaria, ingawa naye bado anahitaji kuwania namba.
Kocha wa Yanga, Hans Pluijm  alisema safu ya ushambuliaji iliyokuwa ikimuumiza kichwa hivi sasa imekamilika kwa asilimia 90.
Mwananchi

No comments: