Advertisements

Sunday, March 24, 2024

KITANDULA AFUNGA MAFUNZO YA ASKARI 298 WA JESHI LA UHIFADHI WALIOHITIMU MAFUNZO YA KIJESHI MLELE


Na Kassim Nyaki, Mlele Katavi.
Naibu waziri wa Maliasili na utalii Mhe. Dunstan Kitandula (Mb) leo tarehe 23 machi, 2024 amefunga mafunzo ya kijeshi wa askari wa jeshi la uhifadhi 298 yaliyofanyika kwa muda wa miezi 6 katika kituo cha mafunzo ya jeshi la Uhifadhi Mlele Mkoani Katavi.

Mafunzo ya askari hao 298 yamehusisha taasisi tatu za uhifadhi ambazo Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) yenye askari 81, Wakala wa huduma za Misitu (TFS) wenye askari 96 na Mamlaka ya usimamizi wa Wanyamapori (TAWA) yenye askari 121.

Akitoa taarifa ya mafunzo mkuu wa Mafunzo hayo Kanali Henry Komba ameeleza kuwa mafunzo hayo yaliyoanza tarehe 1 oktoba 2023 askari wamefundishwa mada mbalimbali zikiwemo usalama wa habari na mawasiliano, ukamataji wa wahalifu, upelelezi, amri za jumla za Jeshi la Uhifadhi, itifaki za kijeshi, uzalendo, usomaji wa ramani, utalii na huduma kwa wateja pamoja na matumizi ya silaha mbalimbali.

Naibu katibu wizara ya Maliasili na utalii Kamishna wa Polisi Benedict Wakulyamba amewaelekeza askari waliohitimu mafunzo kuhakikisha wanajituma kulinda maliasili, kupambana na wahalifu na kuzingatia misingi ya sheria, kanuni na haki za binadamu katika ulinzi wa rasilimali za wanyamapori na misifu.

Akifunga mafunzo hayo Naibu waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dunstan Kitandula amewaelekeza askari wote waliohitimu kuishi kwa vitendo mafunzo waliyoyapata, kujiepusha na utovu wa nidhamu pamoja na vitendo vya rushwa ili kulinda viapo vyao.

"Pamoja na kujiepusha na vitendo vya rushwa katika kutekeleza majukumu yenu hakikisheni mnazingatia misingi mikuu mitatu ambayo ni nidhamu, uadilifu na uaminifu" ameongeza Mhe. Kitandula
Mwakilishi wa Kamishna wa Uhifadhi NCAA, Afisa Uhifadhi Mwandamizi Donatus Gadiye amewaasa askari kujiandaa kikamilifu katika ulinzi, uhifadhi na kukabiliana na vitendo cha kihalifu ikiwemo changamoto za uhalifu hasa ujangili katika maeneo ya hifadhi ili kuimarisha usalama wa rasilimali za nchi.

Mafunzo yametolewa na wakufunzi kutoka Jeshi la wananchi, jeshi la polisi na jeshi la uhifadhi.

No comments: