Wednesday, May 29, 2024

MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR MHE.HEMED SULEIMAN AFUNGUA MAKUMBUSHO YA AMANI NA VIUMBE HAI MNAZI MMOJA JIJINI ZANZIBAR

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Abdulla akikata Utepe kuashiria Ufunguzi wa Makumbusho ya Amani na Viumbe Hai katika Eneo la Mnazi Mmoja jijini Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Abdulla akipokea maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Kale Bi. Maryam Mansab wakati wa Ufunguzi wa Makumbusho ya Amani na Viumbe Hai katika Eneo la Mnazi Mmoja jijini Zanzibar.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar MHE. HEMED SULEIMAN ABDULLA amesema Makumbusho ya Amani na Viumbe Hai yatasaidia katika kukuza Sekta ya Utalii na kukuza uchumi wa nchi kwa vile ni kivutio kikubwa cha wageni walio wengi wanaoitembelea Zanzibar.

Ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa Makumbusho ya Amani na Viumbe hai yaliyopo Mnazi Mmoja jijini Zanzibar.

Amesema Serikali imejipanga kufanya ukarabati katika maeneo yote ya kihistoria ikiwemo eneo la kihistoria la Fufuni Pemba, Msikiti wa Kihistoria wa kichokochwe Pemba, eneo la kihistoria la Maruhubi pamoja na Mahamamu ya Forodhani, Kijichi, Hamamni na Kizimkazi Unguja kwa lengo la kukuza sekata ya utalii pamoja kuengeza pato la nchi.

Mhe. Hemed amefahamisha kuwa Serikali kupitia Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale itaendelea kuyaendeleza maeneo ya kihistoria kwa kuzungusha ukuta, Uwekaji wa vitu vya kale, kuyajenga ili kurudisha uasili wake sambamba na kuimarisha majengo ya utoaji wa huduma kama vile vyoo, migahawa na maduka.

Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar amesema kwa kutambua na kuthamini umuhimu mkubwa wa Makumbusho, Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2020-2025 imechukua hatua ya kuweka mazingira mazuri katika maeneo ya Makumbusho kwa kutunga Sheria ya Uhifadhi wa mambo ya kale No.11 ya mwaka 2022 inayosimamia kutunza, kuhifadhi na kuendeleza Makumbusho ya Mambo ya Kale.

Aidha Mhe. Hemed amewataka wafanyakazi wa Makumbusho ya Amani na viumbe hai pamoja na Makumbusho mengine kuendelea kuyaimarisha na kuyatunza ili yaendelee kuwa kivutio cha wageni wengi zaidi wa ndani na nje ya nchi.

Sambamba na hayo, Mhe. Hemed ametoa wito kwa jamii kutokuyavamia maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya Makumbusho ya historia na badala yake waendelee kushirikiana na Serikali katika kuyalinda na kuyaimarisha ili kuendelea kuongeza vivutio vya utalii Zanzibar sambamba na kuwataka kujenga tabia ya kutembelea maeneo ya Makumbushoya kihistoria ili kujifunza mambo mbali mbali ya kihistoria katika nchi yetu.

Nae Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar MHE. MUDRIK RAMADHAN SORAGA amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha inahuwisha Sekta ya Utalii na Mambo ya Kale kwa kuyafungua Makumbusho yote ambayo yalikuwa hayafanyi kazi ndani ya Zanzibar.

Amesema Serikali kupitia Wizara ya Utalii imejipanga katika kuyajenga na kuyafanyia ukarabati maeneo ya Kihistoria na maeneo mengine ambayo ni vivutio vya Watalii ili kurejea katika hadhi yake jambo ambalo litapelekea kukuza pato la mtu mmoja mmoja na la Taifa kwa ujumla.

Akisoma taarifa ya Kitaalamu juu ya Uzinduzi wa Makumbusho ya Amani na Viumbe Hai, Katibu Mkuu Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale Dkt. ABOUD SULEIMAN JUMBE amesema kupitia mradi wa kuhifadhi na kuendeleza maeneo ya urithi Serikali imeamua kuyafanyia ukarabati na kuimarisha maonesho ya Makumbusho ili kutarejesha katika haiba yake hasa kwa vile baadhi yao ni urithi muhimu wa Kitaifa na Kimataifa.

Dkt. Jumbe amesema kuwa Makumbusho ya Amani na Viumbe Hai yana umuhimu mkubwa katika uimarishaji wa Elimu na Utafiti, kuchangia uimarishaji wa Utalii wa ndani na nje katika kukuza uchumi wa nchi pamoja na kuhakikisha uhifadhi wa urithi wa kihistoria na kiutamaduni kwa vizazi vijavyo.

Zaidi ya shilingi Bilioni saba(7) zimetumika katika ukarabati wa Makumbusho hayo kwa kuzifanyia ukarabati kuta na sakafu ndani na nje, ujenzi wa mabanda ya viumbe haipamoja na urejeshaji wa viumbe hai, ukarabati wa maabara pamoja na uwekaji wa vifaa vya teknolojia ya habari na mawasiliano ambavyo vitatumika katika kutoa elimu kwa wageni.

Imetolewa kitengo cha Habari (OMPR)
Tarehe …29.05.2024

No comments: