Advertisements

Monday, June 3, 2013

WADUDU NI CHAKULA BORA!

Senene.
Wadudu ni chanzo kikubwa cha protini, mafuta mazuri kiafya, madini na kamba lishe. Aidha, wadudu wameelezwa kuwa ni rafiki wa mazingira na ni rahisi kuwafuga au kuwakamata.
Inakadiriwa na shirika hilo kuwa kiasi cha watu bilioni 2 duniani wanatumia wadudu kama sehemu ya milo yao ya kila siku. Imeshauriwa watu kupendelea kula wadudu kutokana na ukweli kwamba protini inayopatikana kwenye wadudu hao ni bora zaidi kuliko ile inayopatikana kwenye nyama ya kuku, ng’ombe, nguruwe na samaki.
Mbali ya wadudu kuwa ni chanzo kikuu cha protini na mafuta mazuri kama ya samaki (fish oil), lakini pia ni chanzo kizuri cha madini ya kashiamu (calcium), chuma (iron), seleniamu (selenium), zinki (zinc) na Vitamini B

WADUDU WA TANZANIA
Kuna aina zaidi ya elfu tisa ya wadudu wanaoliwa sehemu mbalimbali duniani. Lakini kwa nchini Tanzania, kuna aina kuu mbili za wadudu ambao wanajulikana na kutumiwa kama sehemu ya kitoweo katika familia nyingi nchini, hasa vijijini.
Aina hizo mbili maarufu nchini Tanzania ni Senene na Kumbikumbi, ambao hupatikana kwa wingi zaidi nyakati za masika sehemu za vijijini. Senene na Kumbikumbi ni miongoni mwa vyakula vyenye faida nyingi mwilini na ni vitamu pia.
Kutokana na kuwa na faida nyingi za kiafya mwilini, ndiyo maana wamekuwa wakiliwa tangu enzi na enzi na mababu zetu. Ingawa idadi kubwa ya wadudu hao wanaoliwa hupatikana kwa kuwakamata kwenye makazi yao porini, lakini katika siku za hivi karibuni, mifumo ya kisasa ya kuwakamata wadudu hao imebuniwa na hivyo kurahisisha ukusanyaji kwa idadi kubwa na kwa mara moja.
Kwa kuona umuhimu na faida za kiafya zinazoweza kupatikana kwa kula wadudu, Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa limetoa wito kwa nchi zote duniani kufuga wadudu hao kwa wingi kibiashara, shirika linaamini nchi nyingi zikitilia mkazo suala hili, zinaweza kupunguza tatizo la njaa kwa kiasi kikubwa na wakati huo huo kuboresha afya za watu wengi.
Bila shaka hii ni habari njema na ya kutia moyo kwa watu ambao tayari wanafuga na kuvuna Senene kibiashara, kama ambavyo tunavyoona wakiuzwa baadhi ya sehemu za mijini. Nitoe wito kwa watu wengine ambao hawajawahi kuonja Senene au Kumbikumbi kufanya hivyo, kwani siyo tu wana faida kiafya mwilini, bali ni watamu sana. (so delicious)!-GPL

No comments: