
Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Wilson Kabwe amesema uchunguzi wa tuhuma zilizomfanya Rais John Magufuli kumsimamisha kazi jana utabainisha ukweli huku akihoji; “ikiwa itabainika kwamba nilionewa nitalipwa fidia?”
Alisema hayo mara baada ya Dk Magufuli kutangaza kumsimamisha kazi wakati wa uzinduzi wa Daraja la NSSF Kigamboni ambalo sasa litaitwa Daraja la Nyerere baada ya kumwita Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kueleza tuhuma dhidi ya mkurugenzi.
Alipoulizwa jana, Kabwe alisema hakuwa na taarifa za kusimamishwa kwake na mazungumzo yake na mwandishi wetu yalikuwa kama ifuatavyo:
Mwandishi: Habari mkurugenzi?
Kabwe: Salama.
Mwandishi: Tumepata taarifa za kusimamishwa kwako kazi na Rais kutokana na tuhuma zilizotolewa juzi na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Makonda tunaomba maoni yako.
Kabwe: Sijasikia ndiyo kwanza unaniambia wewe, kasema lini Rais?
Mwandishi: Leo wakati akizindua Daraja la Kigamboni.
Kabwe: Alitamka palepale au?
Mwandishi: Ndiyo.
Kabwe: Sasa kama ameshasema yeye ndiyo mkubwa mimi sina la kusema tena.
Mwandishi: Nataka kujua unazungumziaje uamuzi huo?
Kabwe: Nimekwambia sina la kukwambia kwa sasa lakini nimesema tu sina shida na hilo, uchunguzi ufanyike nina uhakika ukweli utajulikana tu. Lakini kama ukijulikana na ikibainika nimeonewa je, kuna fidia yoyote nitalipwa?
1 comment:
Imefika wakati sasa kwa Tanzania kama Taifa kutambua michango ya watu (Wananchi) au jamii nyengine kwa taifa letu hatuwezi kugeuka na kuwaapuuza wengine mchango au michango yao mikubwa kwa ukombozi na maendeleo ya taifa hili na kupachika jina la kila kitu kikubwa ni Nyerere huo ni upofu,Nyerere hakuwa Mungu wa Tanzania, Nawaomba wale wenye mamlaka hiyo kutambua kuwa wapo wengine walitowa mpaka roho zao kwa nchi hii yetu sote ya Tanzania, Mungu Wabariki Watanzania
Post a Comment