Advertisements

Wednesday, February 22, 2017

MWANAFUNZI AKIPATA MIMBA MZAZI JELA MIAKA 30

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, amesema serikali itatoa adhabu kali ya kifungo cha miaka 30 jela kwa wazazi wote wawili wa mtoto wa kike atakayekatishwa masomo na kulazimishwa kuolewa ama akipata ujauzito.

Aidha amesema Serikali itamfunga jela miaka 30 kijana anayetaka kumuoa msichana anayesoma pamoja na wazazi wake.

Amesema Serikali ya awamu ya tano imedhamiria kumlinda mtoto wa kike katika kuhakikisha kuwa anapata haki yake ya msingi ya kusoma kufikia elimu ya chuo kikuu kwa kujenga mabweni na kuwachukulia hatua kali za kisheria watu watakaowapa mimba na kuwaozesha katika umri mdogo na kukatisha masomo yao.

Majaliwa aliyasema hayo jana wilayani Hanang, mkoani Manyara katika ziara yake ya kikazi ya siku sita kwa mkoa huo.

Alisisitiza kuwa kupitia sera ya kuboresha elimu nchini serikali imeondoa michango ya fedha za kulipia bili za maji, umeme, gharama za mlinzi na mitihani ili kumpunguzia gharama mzazi na mlezi na kuwaacha wazazi kushughulikia maeneo mengine muhimu kwa mtoto wao.

Alisema tayari kwa mwaka huu wa fedha, walimu 4,396 wa masomo ya sayansi wameajiriwa ambapo alisisitiza kuwa wazazi na walezi wanalo jukumu kubwa la kusimamia maendeleo ya shule ya watoto wao kwa lengo la kupandisha ufaulu wa elimu kwa wilaya,mkoa na taifa.

“Mtoto akiwa mtoro baba na mama wa mtoto huyo atashitakiwa,mtoto wa kike asiguswe,vijana waendesha bodaboda acheni kuwalaghai watoto hao kwa zawadi na usafiri, tutawasaka wote,” alisisitiza.

Akizungumza na watumishi wa umma katika halmashauri ya wilaya hiyo, aliwataka watumishi hao kujivunia serikali yao kwa kuienzi katika kufanya kazi kwa nidhamu katika kuwatumikia wananchi bila kujali uwezo wao, kabila wala rangi zao kwa kuwa wamepewa dhamana ya kusikiliza kero zao.

Majaliwa alifafanua kuwa wafanyakazi wana wajibu wa kuwatumikia watanzania kwa kuwa wao ni waajiriwa wa serikali hivyo ni muhimu wakatoka maofisini na kwenda vijijini kusikiliza kero na kuzitatua badala ya wananchi kungojea viongozi wa kitaifa kuja kusikiliza kero na malalamiko yao wakati wao ni watendaji wakuu katika maeneo yao.

“Utumishi wenu hauhitaji upendeleo ama ahadi za njoo kesho, utumishi wa awamu ya tano ni wa uwajibikaji zaidi na uwajibikaji ni pamoja na kuwa mwaminifu katika kulinda na kusimamia kikamilifu fedha za serikali zinazotengwa katika halmashauri husika kwa ajili ya maendeleo,” alisema.

Akizungumzia soko la kimataifa la Endagaw, aliwapongeza wananchi wa wilaya hiyo kwa kukubaliwa kujengewa soko kubwa la kimataifa ambako wakulima watapeleka mazao yao na kuyauza lakini pia wataweza kuingiza mapato kwa kukodisha makampuni makubwa yanayohitaji kukodi kuhifadhi mazao kama NRFA.

Aliwataka wakulima wa mazao mbalimbali wilayani Kateshi kulitumia soko la mazao la kimataifa la Endagaw lililojengwa na ofisi yake kuuza mazao yao kwa bei nzuri badala ya kuuza mazao majumbani ambako wamekuwa wakiuza kwa bei ya chini isiyowasaidia kukuza kipato chao.

Alieleza kuwa serikali itaendelea kjuimarisha miundombinu ya soko hilo kwa kujenga eneo la wazi la nje kudhibiti magari makubwa yanayoshusha na kupakia mizigo yasikwame kutokana na matope na kuwa na mizani ya kupimia mazao na magari.

Kuhusu kero ya maji katika mji wa Katesh, alisema marekebisho yanafanyika kurekebisha mashine ya kuvuta maji na kuhakikisha sera ya maji inatekelezwa kwa vitendo katika kumpatia maji kila mwananchi umbali usiozidi mita 400.

Awali katika taarifa yake Mkuu wa Wilaya ya Hanang, Sara Msafiri alimweleza Waziri Mkuu kuwa changamoto kubwa inayoikabili wilaya hiyo ni migogoro ya ardhi, kuanzisha gereza la wilaya kupunguza usumbufu wa kuwapeleka wahalifu Babati, jambo ambalo alisema atalipeleka wizara ya mambo ya ndani lipate kushughulikiwa.

Msafiri aliomba pia kujengewa mahakama ya wilaya ambapo alisema ni mchakato uliopo wa mahakama kuu kujenga mahakama katika ngazi za wilaya hivyo jambo hilo nalo litashughulikiwa.

Mbunge wa Viti Maalum Mkoa, Ester Mahawe alibainisha tatizo la kuwa na shule ya kidato cha tano na sita moja kwa wilaya nzima ambapo alimwomba Waziri Mkuu kutoa kipaumbele katika bajeti zake za elimu ili shule zaidi zijengwe mkoani humo.

Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Manyara, Rose Kamili (Chadema) aliiomba serikali kufuatilia na kuyatolea maamuzi mashamba makubwa ambayo yamekuwa hayaendelezwi na wawekezaji kutoka Ngano Ltd wanayoyamiliki zaidi ya ekari elfu 45 ambapo wamekuwa wakilima ekari elfu 16 pekee na kuacha migogoro ya ardhi baina yao na wananchi na kukosesha mapato ya halmashauri.

Ziara hiyo ilipata baraka za mvua kubwa baada ya ukame wa muda mrefu ilishangiliwa na umati wa watu waliokuwa wakiimba kwa furaha kuashiria Waziri Mkuu kuja na baraka hiyo kuneemesha mazao yao.

Leo Waziri Mkuu anatarajiwa kuhitimisha ziara yake wilayani Babati ambapo pamoja na mambo mengine atafanya majumuisho ya ziara hiyo na kutoa maelekezo ya serikali kwa wananchi na viongozi ngazi ya mkoa.

HABARI LEO

2 comments:

Anonymous said...

Hapa kaongea kama vile game watoto wakike...je kama ni mtoto wake (waziri)na yeye akafungwe? Msichana hawezi kupata mimba bila kuwa na mwanaume. Hivyo wazazi wa pande zote mbili wanahusika. Kenobi mzazi hana kosa lolote hapa.sanasana wawape elimu ya kutosha. Wazazi wawe wakweli (wazi) wanapokuwa wanaongea na watoto wao......no mawazo yangu.

Anonymous said...

Faru Joni amepatikana.!? Hii ya kuwafunga jela umekaaje. Haya ni maswala ya kimaumbile. Hivinkweli.mzazi unaweza kumchunga mtoto asifanye tendo hilo? Itabidi kutafuta makufuli sasa. Watu hatutafanya shughuli za maendeleo badala yake kuchunga ngombe!!