Monday, October 7, 2024

DC KASKAZINI B AFUNGUA MAFUNZO YA WALIMU WA MADRASA MAHONDA


Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini B Unguja Hamid Seif Said akisisitiza jambo wakati akitoa hotuba ya Ufunguzi wa Mafunzo ya Walimu wa Vyuo vya Qur-ani yalioandaliwa na Mtandao wa Vyuo vya Kur-ani Zanzibar(MVUQUZA) ambayo yamefanyika Mahonda Wilaya ya Kaskazini B Unguja.
Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini B Unguja Hamid Seif Said akitoa hotuba ya Ufunguzi wa Mafunzo ya Walimu wa Vyuo vya Qur-ani yalioandaliwa na Mtandao wa Vyuo vya Kur-ani Zanzibar (MVUQUZA) ambayo yamefanyika Mahonda Wilaya ya Kaskazini B Unguja.
Baadhi ya Walimu wa Vyuo vya Qur-ani waliohudhuria katika Hafla ya Mafunzo ya Walimu wa Vyuo vya Qur-ani yaliofanyika Mahonda Wilaya ya Kaskazini B Unguja.
Kiongozi(AMIRI)wa Mtandao wa Vyuo vya Kur-ani Zanzibar(MVUQUZA)Fakih Ali Juma akitoa maelezo kuhusiana na Mtandao wao huo katika hafla ya Mafunzo ya Walimu wa Vyuo vya Qur-ani yaliofanyika Mahonda Wilaya ya Kaskazini B Unguja.
Naibu Katibu Mkuu wa Mtandao wa Vyuo vya Kur-ani Zanzibar(MVUQUZA)akitoa hotuba ya makaribisho kwa Mgeni Rasmi katika Hafla ya Mafunzo ya Walimu wa Vyuo vya Qur-ani yaliofanyika Mahonda Wilaya ya Kaskazini B Unguja.

PICHA NA YUSSUF SIMAI/MAELEZO ZANZIBAR

Na Sabiha Khamis Maelezo
Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini B Unguja Hamid Seif Said amesema walimu wa madrasa wanamchango mkubwa katika kuboresha misingi bora ya maadili katika jamii.

Ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya walimu wa madrasa wanachama wa Wilaya ya Kaskazini "B" katika ukumbi wa Madrasa Mahonda Msuka, amesema walimu wa madrasa mchango wao wa kuwapatia watoto elimu ya akhera ni mkubwa ambao unasaidia katika makuzi yao.

Amesema endapo elimu ya madrasa itatumiwa ipasavyo changamoto nyingi zinaweza kuepukika katika jamii ikiwemo vitendo vya udhalilishaji.

Ameeleza kuwa ikiwepo jamii yenye kuzingatia maadili katika kuwalea watoto kupitia misingi ya dini itasaidia kupata watoto wema na wenye tabia njema.

Aidha, amewataka walimu hao kutovunjika moyo katika utendaji kazi wao pamoja na kutumia hekma katika ufundishaji ili kuiweka nchi katika amani.

Vile vile ameahidi kuviunganisha vyuo vya madrasa ambavyo havujakamilisha usajili ili kuweza kujiunga na jumuiya hiyo ili kuvisaidia madrasa hizo.

Hata hivyo amesema atawashirikisha walimu wa madrasa na maafisa elimu wilaya katika kufanya maamuzi ya kutenga muda wa kupatia wanafunzi muda wa kujifunza elimu ya Dini kupitia madrasa.

Kwa upande wake Naibu Katibu wa Jumuiya ya Mtandao wa Vyuo vya Qur-an Wilaya ya Kaskazini "B" Foum Suleiman Juma amesema mafunzo hayo yatawasaidia walimu wa madrasa kuweza kusimamia majukumu yao ya ufanyaji kazi kwa uadilifu kwa kufuata miongozo na maamrisho ya Mwenyezi Mungu (s.w).

"Ni jukumu la kila mwalimu kufanya kazi kwa uadilifu bila ya kuangalia maslahi ya kidunia ili tuweze kusimama imara katika kutekeleza majumu yetu" alisema Naibu Katibu.

Amewaeleza kuwa endapo walimu wa madarsa watakuwa wakweli katika kusimamia miongozo ya dini katika kupambana na kila maovu na kutangaza yaliyomema itasaidia nchi kupambana na maovu.

Nao washiriki wa mafunzo hayo wamesema mafunzo hayo yatawasaidia katika kuwaweka pamoja walimu wa madrasa ili kuweza kuhamasisha jamii katika kuwepo malezi shirikishi na kuipeleka mbele Dini ya Kiislam.

Aidha amewataka wazazi na walezi kuendeleza ushieikiano katika malezi ya watoto kupata jamii yenye maadili mema.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Mtandao wa Vyuo vya Qur-an Wilaya ya Kaskazini B kwa lengo la kuviweka pamoja vyuo vya madrasa.

No comments: